Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria, akisisitiza kwamba fikra na shule ya fikra ya mwanzilishi mkuu wa Mapinduzi ya Kiislamu bado iko hai na inaendelea, amesema kuwa; kufuata mawazo ya Imam Khomeini (r.a.) ndiyo njia pekee ya kuikomboa dunia na kuiwezesha kuvuka migogoro na changamoto za sasa.
Kwa mujibu wa ripoti ya Kitengo cha Kimataifa cha Shirika la Habari la Hawza, Sheikh Ibrahim Zakzaky katika kongamano la thelathini na saba la “Wiki ya Imam Khomeini” lililoandaliwa na Jumuiya ya Wanafunzi wa Harakati ya Kiislamu katika makazi yake mjini Abuja, alifafanua vipengele vya haiba na fikra za mwanzilishi mkuu wa Mapinduzi ya Kiislamu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyopokelewa kutoka ukurasa wa ofisi ya Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria, Sheikh Ibrahim Zakzaky katika hafla hiyo alimuelezea Imam Khomeini (r.a.) kuwa ni neema ya Mwenyezi Mungu kwa zama za sasa, ambaye alibadilisha fikra za Umma wa Kiislamu na kuleta mabadiliko makubwa na ya msingi katika kiwango cha kimataifa.
Akizungumzia mabadiliko katika dhana ya kungojea (Intidhar) ndani ya shule ya fikra ya Imam Khomeini (r.a.), alisema: Mwanzilishi wa Mapinduzi ya Kiislamu alibadilisha mtazamo wa kijadi na wa kutochukua hatua wa jamii kuhusu suala hili; kwa sababu kungojea katika shule ya Imam si kukaa tu, kunyamaza na kusubiri, bali ni harakati yenye nguvu, yenye uwezo na inayofuatana na matendo, ambayo kabla ya kudhihiri kwa Hadhrat Baqiyyatullah al-A'dham (a.f.) na hata baada ya kudhihiri kwake, inabaki kuwa wajibu juu ya mabega ya watu wote wa Umma.
Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria alisisitiza: Imam Khomeini (r.a.) alibadilisha mtazamo wa dunia kuhusu dini, kiasi kwamba dini ilitambulika kama njia ya kufikia uhuru, heshima na kujitegemea, si kama chombo cha kuwakandamiza na kuwafanya watu wazembe, kama ilivyokuwa ikitangazwa na madola ya kiburi kabla ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu.
Akiendelea kusisitiza kwamba nguvu halisi na za kimada zipo mikononi mwa matabaka ya watu, aliongeza: Mwanzilishi wa Mapinduzi ya Kiislamu aliifundisha dunia kwamba ushindi wa mwisho dhidi ya madhalimu na wenye kiburi hupatikana tu kupitia kupambana na dhulma, kusimama imara katika fitna na kumtegemea Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa dhati. Ndiyo sababu leo maadui wa Uislamu na watawala wa kimataifa wenye mfumo wa ukoloni wanahofia athari ya fikra za Imam miongoni mwa Umma na wanaendelea na juhudi zao za kuzuia kuenea kwa fikra hizi za kimungu.
Akiashiria kwamba Imam Khomeini (r.a.) yuko hai, kwa sababu fikra, njia na shule yake ya fikra bado ipo hai na inaendelea, alibainisha: Katika hali ya sasa hakuna haja ya kuanzisha njia mpya, bali jukumu pekee la Umma wa Kiislamu ni kufuata kwa usahihi na kwa ikhlasi njia yake ya uongofu.
Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria mwishoni alikumbusha: Hii ndiyo fikra ambayo Shahidi Sayyid Khamenei amesimama imara juu yake kwa nguvu na uthabiti; kwa hiyo dunia ya leo, ili iweze kuvuka migogoro, inahitaji kurejea katika fikra za Imam Khomeini (r.a.), kwa sababu fikra hizi ndio njia pekee ya wokovu na mafanikio ya mataifa.
Maoni yako